Tuesday, October 18, 2016

MAJIMAJI YAMPA MATUMAINI KALLY.

Kalimangonga''Kally''Ongara kocha wa Majimaji.
 Baada ya kuwa na mwanzo mbaya wa msimu timu ya Majimaji ya Songea imempa ahueni kocha wake Kally Ongara baada ya kuibuka na ushindi mabao 2-1 dhidi ya Toto Africans ya mjini Mwanza.
Mchezo huo uliochezwa juzi kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza umeweza kuwapa ahueni ya matumaini timu hiyo ambayo iko kwenye hatua mbaya kimsimamo kwenye ligi.

Mabao ya Majimaji katika mechi hiyo yalifungwa na Peter Mapunda katika dakika ya 30 na 80 huku bao la Toto likifungwa na Reliant Lusajo katika dakika ya 11.

"Mchezo umeisha nadhani pointi tatu ndio muhimu kwetu tulipoanza ligi tulikuwa tumecheza sana chini ya kiwango, lakini tumeweza kufanya mabadiliko tukasisitiza vijana wawe wapambanaji, tulipata mwanzo mgumu kutokana na tumeingia kambini wiki moja kabla ya Ligi Kuu kuanza lakini sasa tunabadilika siku hadi siku,” alisema Kocha Kally.

Alisema amefurahishwa na vijana wake kwa kutengeneza nafasi nyingi katika mechi hiyo ambapo mashuti yao mengine yalikuwa yakigonga mwamba.

"Tulikuwa nyuma ya goli moja tumepambana na kuweza kusawazisha kisha kushinda mechi yetu. Nawaonya wachezaji wangu hakuna mtu mwenye namba yake na pia bado tuna kazi kubwa sana ya kupambana na kushinda dhidi ya African Lyon,” alisema.

Kocha wa Toto, Khalfan Ngassa aliwalaumu wachezaji wake na kusema hawajitambui na wanashindwa kucheza mpira na kuwakilisha mkoa wao. Ngassa mpaka sasa ameiongoza Toto katika mechi tatu na kupoteza mbili dhidi ya Majimaji na Mbao FC huku akishinda moja dhidi ya Kagera Sugar.

No comments:

Post a Comment