Wednesday, October 19, 2016

TBF YAHIMIZA MAANDALIZI KOMBE LA TAIFA.

 
Moja ya timu ya kikapu nchini.

SHIRIKISHO la Mpira wa Kikapu Tanzania (TBF) limehimiza timu kuendelea kufanya maandalizi kwa ajili ya kushiriki mashindano ya Kombe la Taifa yanayotarajiwa kuanza Novemba 11- 26 mwaka huu.


Akizungumza na gazeti hili jana Kamishna wa Ufundi na Uendeshaji wa Mashindano wa TBF, Manase Zablon alisema timu nyingi zimekuwa na desturi ya kufanya maandalizi mafupi matokeo yake zinapokutana ushindani unakuwa mdogo.

Alisema timu zinatakiwa kujifunza kutokana na makosa kwa kuhakikisha maandalizi yao yanaanza sasa.

“Ili timu zifanye vizuri ni muhimu kwao kuanza maandalizi mapema, kujiimarisha ili mashindano yanapofika kila timu ionyeshe ubora, tunahitaji ushindani wa hali ya juu kupata washindi bora,” alisema.

Zablon alisema mashindano hayo yana umuhimu kwani ndiko sehemu wachezaji wa timu za taifa huangaliwa na kuchaguliwa kwa kuwa hujumuisha timu nyingi na zile za mikoani.

Hivi karibuni timu za Tanzania zilishindwa kufanya vizuri katika mashindano ya Afrika Mashariki na Kati Kanda ya tano yaliyofanyika Dar es Salaam, huku Zablon akisema sababu ni timu kushindwa kufanya maandalizi ya kutosha ya muda mrefu.

Alisema timu zote zinahitaji kubadilika na kujifunza kutokana na makosa, kwa ajili ya kufanya vizuri wakati ujao.

No comments:

Post a Comment