Wednesday, October 19, 2016

VPL KUTIMUA VUMBI LEO-YANGA NA AZAM KUSAKA POINTI TATU.


Leo Ligi Kuu Tanzania Bara itaendelea kwenye viwanja tofauti huku timu za Yanga na Azam zikiwa na kibarua cha kutafuta pointi tatu katika michezo yao ya leo ya Ligi Kuu  baada ya timu zote hizo kutoka sare kwenye mechi yao iliyopita iliyowakutanisha.
Yanga itakaribishwa na Toto Africans kwenye uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, wakati Azam FC itakuwa na mchezo mgumu utakaochezwa kuanzia saa moja jioni kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi dhidi ya Mtibwa Sugar.

Timu zote hazina matokeo mazuri yaliyopita, kila mmoja ni lazima itacheza mchezo wa kumaliza hasira ilimradi kupata pointi ambazo zitawasogeza karibu na kinara wa ligi, Simba inayoongoza kileleni mwa msimamo kwa pointi 23.
Huku Yanga mshambuliaji wao Amis Tambwe aliyekuwa majeruhi na kurudi kwa kiungo mchezeshaji Haruna Niyonzima aliyekuwa na matatizo ya kifamilia, huenda kukaendelea kuleta matumaini mapya ya kupata ushindi katika mchezo huo.
Wachezaji Juma Abdul aliyeumia kwenye mchezo uliopita dhidi ya Azam FC, Malimi Busungu aliyedaiwa kuwa ana matatizo ya kifamilia wakati Ali Mustafa anauguza jeraha watakosekana kwenye mechi ya leo.
Yanga na Toto ni timu ambazo zimekuwa zikihusishwa kuwa na uhusiano wa karibu na hasa kwa vile viongozi wa Toto kudaiwa kuwa na mapenzi na timu hiyo ya Jangwani. Mechi ya msimu uliopita baadhi yao walijiweka pembeni mpaka baada ya mechi hiyo wakidai kuwa Yanga damu, hali iliyosababisha baadhi yao kusimamishwa uanachama.
Mechi nyingine itakayochezwa leo ni Azam FC dhidi ya Mtibwa Sugar.

Timu hiyo ya Chamazi imetoka kufanya vibaya katika michezo mitatu iliyopita, ikilazimishwa sare ya bila kufungana dhidi ya Yanga, ikifungwa na Stand United bao 1-0 na sare dhidi ya Ruvu Shooting 2-2. Bila shaka kutokana na kiwango bora katika mechi yao iliyopita, huenda wakaendeleza mapambano na kuhakikisha wanashinda.

Mchezo mwingine utakuwa kati ya Ruvu Shooting inaikaribisha Mwadui kwenye uwanja wa Mabatini Mlandizi.

Maafande hao hawako vibaya sana wanashika nafasi ya sita wakiwa na pointi 13 katika michezo tisa waliyocheza. Mwadui inashika nafasi ya tatu kutoka mwisho kwa pointi tisa baada ya kushinda michezo miwili kati ya tisa, mitatu ikitoka sare na kupoteza minne. Pia, Ndanda inaikaribisha Mbeya City kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona.
Timu hii mara nyingi huwa haikubali kufungwa kwenye uwanja wake wa nyumbani, iko radhi ishinde au kutoka sare, Mbeya City itakuwa na kazi nzito. Timu zote zimecheza michezo 10, zikivuna jumla ya pointi 12 kila mmoja, City ikishika nafasi ya tisa na Ndanda ya 10 kwenye msimamo.
Stand United inashika nafasi ya pili kwenye msimamo ikikimbizana na Simba, kwa tofauti ya pointi tatu, wao wakiwa na pointi 20. Leo itakuwa ugenini kwenye uwanja wa Sokoine Mbeya kumenyana na Prisons inayoshika nafasi ya 11 ikiwa na pointi 1. Mechi ya wawili hawa huwa haitabiriki na leo kila mmoja anahitaji matokeo.
African Lyon itakuwa mwenyeji wa Majimaji. Licha ya Majimaji kushinda mchezo wa mwisho dhidi ya Toto bado inaendelea kushika mkia ikiwa na pointi sita. Bila shaka kama inataka kujikomboa ni lazima ipambane kujiokoa ilipo kwa kushinda mechi zake. Lyon inahitaji kushinda bado ipo na pointi 10 katika nafasi ya 12.

No comments:

Post a Comment