Saturday, October 29, 2016

VPL WIKIENDI HII-SIMBA KUENDELEZA REKODI KAMBARAGE LEO?


Klabu ya mtaa wa Msimbazi SIMBA SC leo itakuwa ugenini kwenye Uwanja wa CCM Kambarage dhidi ya Mwadui ikiwa ni mchezo wa pili kwa timu hiyo kucheza nje ya Dar es Salaam baada ya ule dhidi ya Mbeya City, ambapo waliibuka na ushindi wa mabao 2-0. . Mwadui ambayo iko nafasi ya tisa kimsimamo wiki iliyopita waliibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Ndanda.

Simba itakuwa kwenye Uwanja wa CC-M Kambarage, Shinyanga  kukabiliana na timu ya Mwadui kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya soka ya Tanzania Bara.

Simba ambayo haijapoteza mchezo hata mmoja tangu ligi hiyo ilipoanza Agosti mwaka huu, ambapo tayari wameshacheza mechi 11, ikishinda mechi tisa na kutoka sare mara mbili ikiwa kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo. Kama Simba itaibuka na ushindi kwenye mchezo wa leo dhidi ya Mwadui ya Shinyanga, itazidi kujiimarisha kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo na kujitengenezea mazingira mazuri ya kushinda taji hilo kwa mara ya kwanza kwa takribani miaka minne iliyopita.

Mchezo huo ambao unaonekana kuwa mgumu kwa timu zote mbili kwani Mwadui haijawahi kufungwa na Simba kwenye Ligi Kuu Vodacom Tanzania Bara  na mchezo huo unachezwa nyumbani hivyo Simba watakuwa na kibarua kizito kuweza kuendeleza rekodi yao ya kutopoteza mchezo. Huku kocha wa Simba Joseph Omog akisema mechi hiyo itakuwa ngumu kwani kwani wapinzani wao wanatumia mabavu uwanjani, lakini watapambana ili kuhakikisha wanaibuka na ushindi. Omog alisema hana wasiwasi na kikosi chake, kipo vizuri, akihofia ubaya wa viwanja vya mikoani ambavyo alisema vinaweza kuwaathiri wachezaji wake, wasicheze kwa uhuru.

“Tumejiandaa vizuri kushinda, nimewaona wapinzani wetu ni wazuri, lakini wanacheza soka la nguvu, hivyo wachezaji wangu wanatakiwa kuwa tayari kukabiliana nao kwa aina ya soka. 

Huku kocha msaidizi wa timu ya Mwadui, Khalid Adam alisema jana kuwa wamewasoma Simba na wanajua wapi wawakamate, hivyo haitakuwa mechi rahisi kama mashabiki wa Simba wanavyodhani kwamba wanakwenda kuchukuwa pointi tatu kwao na kuondoka.

“Sidhani kama kuna sababu ya kuwahofia Simba, timu zote zinacheza kwa kujituma kutokana na changamoto iliyopo ya ushindani wa msimu huu, tunapeana maelekezo ya kuzingatia wawapo uwanjani wafanye nini kupata ushindi, tulianza vibaya ila sasa tunakwenda vizuri,” alisema Khalid.

Mechi nyingine za leo zitakuwa ni; Mbeya City itaikaribisha Maji Maji kwenye uwanja wa Sokoine, wakati JKT Ruvu itakuwa mwenyeji wa Ndanda huku African Lyon ikiwakaribisha Prisons, Toto watakuwa wenyeji wa Mtibwa Sugar.


No comments:

Post a Comment